Ijumaa, 26 Desemba 2014

MGOGORO WA WAFANYABIASHARA SOKO LA NEWALA

MGOGORO WA WAFANYABIASHARA SOKO LA NEWALA WAPATIWA UFUMBUZI WA MUDA

  • ULIHUSU USHUSHAJI WA MIZIGO ENEO LA SOKO
  • ULIPELEKEA WAFANYABIASHARA KUGOMA KWA SIKU MBILI
Mgogoro uliokuwa umeanza kuibuka katika soko kuu la wilaya ya Newala baina ya wafanyabiashara wa soko hilo kwa upande mmoja na Serikali kwa upande mwingine sasa umepatiwa ufumbuzi wa muda. Mgogoro huo ulianza pale  mamlaka ya mji mdogo wa Newala ilipotoa agizo kwamba malori yote makubwa ya mizigo sasa hayataruhusiwa kushusha mizigo katika barabara zinazozunguka soko hilo ambalo lipo katikati ya mji. Sababu kubwa iliyotolewa ni ufinyu wa maeneo yenyewe ya kushushia hali ambayo inasabisha msongamano mkubwa na inaweza kusababisha hata ajali. Hivyo iliamriwa kwamba sasa magari yote makubwa yatashushwa eneo la pembeni ya stendi kuu ya mabasi yaendayo sehemu mbalimbali kutoka hapa wilayani ambapo ni zaidi ya kilometa mbili kutoka lilipo soko na baada ya hapo mizigo hiyo ibebwe na magari madogo mpaka sokoni.

Kitendo hicho hakikuwafurahisha wafanyabiashara wa soko hilo ambapo madai yao makubwa yalikuwa kwanza ni umbali ambao unasabisha kuongezeka kwa gharama na pia eneo lenyewe si salama na halina hata sehemu ya kuhifadhia mizigo. Walidai kuongezeka kwa gharama hizo za kufikisha mizigo kutapelekea wao kupandisha bei ya bidhaa na hivyo kumuathiri zaidi mnunuzi ambaye ni mwananchi wa kawaida.

Kaimu mkuu wa Mkoa akiongea na wafanyabiashara
Mvutano huo ulipelekea wafanyabiashara wa soko hilo kuandika barua kwenda Halmashauri wakitoa mpaka tarehe 22 ya mwezi huu Desemba kushughulikia madai yao, lakini ilipofika tarehe hiyo huku wakiwa hawajapata majibu yoyote ndipo wakaamua kugoma kufungua biashara zao kwa siku mbili yaani tarehe 22 na 23 ya mwezi huu. Mgomo huo ulipelekea Serikali kuitisha kikao cha wafanyabiashara wote siku ya tarehe 23 mwezi huu na kuendeshwa Kaimu mkuu wa Wilaya ya Newala ambaye pia anakaimu nafasi ya mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mkuu wa wilaya ya Tandahimba Mheshimiwa Ponsiano Damiami na kuhudhuriwa na idadi kubwa ya wafanyabiashara hao.Baada ya kikao hicho wafanyabiashara walifungua biashara zao kuanzia kesho yake yaani tarehe 24 na hivyo kuwawezesha watu kujipatia mahitaji yao ya kila siku ikiwemo maandalizi ya sikukuu za Krismasi na Mwaka mpya.


Kaimu mkuu wa Mkoa huyo kwanza aliamua kwenda kutembelea eneo walilotengewa wafanyabiashara kwa ajili ya kushushia mizigo na kuahidi kutoa tamko ndani ya siku mbili. na kuanzia siku ya Tarehe 25 Desemba uamuzi umefikiwa kwamba sasa magari yote makubwa yatashushia mizigo yao eneo la Shirika la maendeleo la Newala (NEDECO)ambalo lipo kama mita mia mbili hivi kutoka sokoni huku ufumbuzi wa kudumu ukiendeela kutafutwa. Kwa mujibu wa diwani wa kata ya Mtonya Mheshimiwa Masoud Ismael Mbelenje tayari swala hilo limekwishaanza kutafutiwa ufumbuzi katika ngazi husika za wilaya.

Biashara zikiendelea kama kawaida
Uamuzi huo umeonekana kuwaridhisha kwa kiasi wafanyabiashara hao huku wakiwa wana matumaini ya kupata ufumbuzi wa kudumu. Bwana Hamis Namata ni muuzaji maarufu wa viungo vya chakula na madawa ya asili sokoni hapo anasema uamuzi huo umekuwa ni nafuu kwao kwani angalau sasa wanashusha mizigo karibu na maeneo ya biashara zao. Hata hivyo amezitaka mamlaka husika kuangalia jinsi ya kuboresha miundombinu ya eneo husika kwani hivi sasa hakuna hata sehemu ya kuhifadhia mizigo pindi inaposhushwa. Amesema hii itakuwa tatizo endapo mvua itaanza kunyesha na kupelekea uharibifu wa bidhaa kwani hakuna pa kuhifadhi, lakini alimaliza kwa kusema ana matumaini ufumbuzi wa kudumu utapatikana.

Mizigo ikishushwa na kupakiwa kwenye magari madogo
 Hivi sasa magari makubwa yameonekana yakishusha mizigo katika eneo hilo la NEDECO na maeneo mengine nje ya mji na kufanya barabara zinazolizunguka soko kuu kuonekana magari madogo maarufu huku kwa jina la vikeri (yaani carry) yakishusha mizigo, na hii kwa upande mwingine imekuwa ni faida kwa wenye magari madogo maana biashara imeongezeka sasa kwao tofauti nahapo nyuma magari makubwa yalipokuwayanashushia nje ya soko.

Kwa upande wa wananchi wa kawaida wengi wamefurahishwa na uamuzi wa kuendelea kufunguliwa kwa soko, kwani kwa siku mbili za tarehe 22 na 23 ambapo soko halikufunguliwa ilikuwa ni adha kubwa kwao katika kujipatia mahitaji yao ya kila siku.



Hakuna maoni: